Jumapili , 2nd Dec , 2018

Meya wa Jiji la Dar es salaam, Isaya Mwita jana Jumamosi Desemba Mosi, 2018 alikamatwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, ambpo kwa mujibu wa ripoti anaendelea kushikiliwa hadi sasa.

Meya wa Jiji la Dar es salaam, Isaya Mwita.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, Lazaro Mambosasa amesema kuwa sababu ya Mwita kukamatwa ni kitendo chake cha kuongoza maandamano bila kuwa na kibali.

Tulipomkamata akaeleza alikuwa anakwenda kuzindua kisima cha maji ambacho hakukijenga yeye kilijengwa na serikali kupitia kwa mheshimiwa DC aliyehamia Ruangwa. Sasa yeye alikuwa anataka kupora ili kutafuta sifa kwamba alijenga yeye wakati mradi ni wa Serikali, aliokuwa amewaalika walikimbia wote,” amesema Mambosasa.

Aidha Kamanda Mambosasa amesema kuwa Jeshi la Polisi linaendelea kumshikilia Meya huyo hadi pale upelelezi utakapokamilika, baadaye atafikishwa mahakamani.

Kwa upande wao CHADEMA kupitia Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje wa chama hicho, John Mrema amesema Meya huyo jana alikuwa na mkutano na baadhi ya wananchi wa kata ya Vijibweni kabla ya kuzindua matawi mapya, ambapo walipokuwa wakielekea katika uzinduzi wa matawi hayo polisi waliwavamia na kuwakamata.

Manadamano hayo yalifanyika katika kata ya Vijibweni, wilayani Kigamboni kuelekea daraja la Mwalimu Nyerere, ambapo Meya Mwita pia ni diwani wa kata ya Vijibweni Kigamboni kwa tiketi ya CHADEMA.