Jumatano , 8th Jul , 2020

Aliyewahi kuwa Mbunge wa Arumeru kupitia CHADEMA Joshua Nassari, amewaomba radhi wale wote waliokuwa wakitamani kumuona yeye akiendelea kuwa upinzani, kwa kusema hawezi kuwa mnafiki, huku akikishukuru chama chake cha awali kwa kumlea tangu akiwa mdogo.

Joshua Nassari

Nassari ametoa kauli hiyo hii leo Julai 7, 2020, wakati akitangaza rasmi kuhamia CCM na kupokelewa na Mwenyekiti wa UVCCM Kheri James, na kuongeza kuwa atakuwa ni mnafiki kama ataendelea kumpinga Rais Magufuli kwa kuwa yale yote aliyokuwa akiyapigania yeye yamekwishakamilishwa.

"Ninawashukuru sana CHADEMA kwa kunilea na kunifikisha hapa nilipo leo hii, naomba Watanzania wote wanaonisikiliza kwa moyo wa dhati kabisa, wale ambao wanakwazwa kwa sababu walitamani kuniona nikiwa upinzani naombeni mnisamehe, siwezi kuendelea kuwa mnafiki roho yangu imekataa, sijaja kama mgombea na sijachukua fomu popote nimekuja kuunganisha nguvu" amesema Nassari.

Joshua Nassari alivuliwa Ubunge wake na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai, kutokana na vitendo vyake vya kutokuhudhuria vikao vitatu vya Bunge mwaka 2019.