Alhamisi , 14th Mar , 2019

Mkuu wa mkoa wa Singida, Bi. Rehema Nchimbi, amekanusha taarifa za kuitaka serikali kuhalalisha biashara ya ngono, ili kuongeza mapato katika mkoa wake na taifa kwa ujumla.

Akizungumza na www.eatv.tv. Rehema Nchimbi amekana kuhusika na taarifa hiyo akisema kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu, hivyo hilo ni suala ambalo hawezi kulifanya kamwe.

Akiendelea kuzungumzia hilo Bi. Rehema amesema kwamba mkoa wa Singida uko mstari wa mbele kupinga biashara hiyo huku wakiwa na lengo kwa kuikomesha kabisa, baada ya kuwakamata wanawake wanaofanya biashara ya ngono ambao wanatarajiwa kufikishwa kizimbani hii leo.

Asimulia 

“Nitetee ufuska?, mimi mtumishi wa Mungu, Mshauri wa Askofu kanisa la Anglikana Tanzania, aliyesema hizo taarifa ni mpumbavu, kuna operesheni kubwa katika mkoa wa Singida ya kuwakamata, nafikiri leo au kesho watafikishwa mahakamani, tutawakamata sawa sawa, na yeyote atakayejihusisha nao hao machangudoa tutamkamata, Singida sio ya machangudoa”, amesema.

Hapo jana kumekuwa na taarifa zilizosambaa mitandaoni zinazosema kwamba Mwenyekiti wa Halmashauri ya Iramba mkoani Singida, Ndg. Simon Tyosela ameishauri serikali kuhalalisha biashara ya akina dada wanaoujiuza, maarufu machangudoa, jambo ambalo liliungwa mkono na mkuu huyo wa mkoa.