Jumanne , 21st Jan , 2020

Hakimu Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Janeth Mtega, ameutaka upande wa Mashtaka katika kesi ya uhujumu uchumi, inayomkabili Afisa wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu(LHRC), Tito Magoti na mwenzake kuhakikisha Februari 5, 2020, wanaeleza upelelezi wa kesi hiyo umefikia wapi.

Tito Magoti akiwa na mwenzake Theodory Giyani, katika viunga vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Hayo ameyabainisha leo Januari 21, 2020, wakati kesi hiyo ilipofikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa, ambapo upande wa mashtaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Monica Mbogo, ulidai kuwa upelelezi huo umefikia katika hatua nzuri na kuomba kesi hiyo iharishwe na kupangiwa tarehe nyingine.

Baada ya hayo yote, Hakimu Mtega, aliiahirisha kesi hiyo, hadi Februari 5, na watuhumiwa hao wamerudishwa rumande kutokana na kuwa mashtaka yanayowakabili kutokuwa na dhamana.

Tito Magoti na mwenzake Theodory Giyani, wanakabiliwa na mashtaka matatu, ikiwemo utakatishaji wa pesa kiasi cha shilingi milioni 17, kushiriki genge la uhalifu pamoja na kumiliki programu ya kompyuta iliyotengenezwa kwa ajili ya kufanya uhalifu.