Alhamisi , 26th Sep , 2019

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, imemuhukumu adhabu ya kifo mkazi wa Kata ya Chikonji, Manispaa ya Lindi, Mohamedi Hassani Omari (45), baada ya kukutwa na hatia ya mauwaji ya kukusudia dhidi ya Andrew Ndemba (Mtanzania) kisa alimnyima supu ya kuku.

Hukumu hiyo imetolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Paul Ngwembe, baada ya ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka kuthibitishwa bila kuacha Shaka yeyote.

Jaji Ngwembe akitoa hukumu katika kesi hiyo namba 48/2016, kupitia kifungu cha Sheria namba 196 kanuni ya adhabu sura ya 16/2002, alimuhukumu Mohamedi Hassani Omari (45), adhabu ya kunyongwa hadi kufa.

Mwanzoni ilidaiwa mahakamani hapo na Mwanasheria wa Serikali, Emmanuel John, kuwa Mohamedi Hassani Omari alifanya mauwaji hayo Aprili 07/2016 usiku,baada ya Andrew Ndemba maarufu (Mtanzania) kukataa kumnunulia Supu ya kuku.

Alisema siku hiyo ya tukio, Mohamedi Hassani Omari akiwa ameongoza na mpenzi wake, walifika nyumbani kwa rafiki yao na walikumkuta marehemu akiwa anakunywa supu ya kuku, na kuomba amnunulie lakini alijibiwa hana fedha.

Wakili John ameeleza kuwa majibu hayo, yalimchukiza mshitakiwa Mohamed ndipo mzozo ulipoanza huku akimpa kauli za vitisho kuwa atamuonyesha, ambapo marehemu alilipiga teke sufuria la supu, kisha kuondoka eneo lile akiwa na rafiki yake Issa Abdallah.

Alisema wakiwa wanaelekea nyumbani kwao, mshitakiwa alichukuwa panga na kwenda kuwavizia njia ambayo walikuwa wakiitumia kupita na walipokaribia eneo alilosimama mshitakiwa aliwasimamisha, na kutekeleza azmio lake la kuuwa.