Jumatano , 30th Jan , 2019

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli amemteua Dkt. Islam Seif Salum Mchenga kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu (Deep Sea Fishing Authority – DSFA).

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli.

Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi imeeleza kuwa uteuzi wa Dkt. Mchenga umeanza tarehe 01 Desemba, 2018 na kwamba kabla ya uteuzi huo alikuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi - Zanzibar.

Wakati huo huo Rais Magufuli amemteua Dkt. Emmanuel Andrew Sweke kuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu (DSFA).

Uteuzi wa Dkt. Sweke umeanza tarehe 01 Desemba, 2018 na kabla ya uteuzi huo alikuwa Afisa Utafiti wa Uvuvi Mwandamizi na Kaimu Mkurugenzi wa Kituo cha Utafiti wa Uvuvi Tanzania (Tanzania Livestock Research Institute - TAFIRI) – Kigoma.

Katika hatua nyingine, Mhe. Rais Magufuli amemteua Prof. Sebastian W. Chenyambuga kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo (TALIRI).

Uteuzi wa Prof. Chenyambuga umeanza tarehe 26 Januari, 2019.

Pia amemteua Prof. Justinian Rwezaula Ikingura kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (Geological Survey of Tanzania - GST).