Jumatatu , 21st Dec , 2015

Serikali imesema kuwa imekwishatenga kiasi cha sh. bilioni 137 kwa ajili ya kugharamia utoaji wa elimu ya bure kuanzia Januari hadi Juni, mwakani ambapo imeshaanza kusambaza pesa hizo katika mashule nchini

Rais wa Jamhuri ya Muungani wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa wakipeana mikono

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati akizungumza na mamia ya wananchi waliofika kumsikiliza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa uwanja wa mikutano wa Likangala wilayani Ruangwa, mkoani Lindi na kuongeza Kazi ya utumbuaji majipu imezaa matunda kwani serikali imeweza kupata fedha za kugahrimia elimu ya bure ambayo iliahidiwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli wakati wa kampeni.

Fedha hiyo tunayo, na tumeshaanza kuisambaza kwa sababu tunataka shule zikifunguliwa Januari, 2016 watoto waanze kufaidika,” alisema huku akishangiliwa.

“Atakayezigusa fedha hizi na kuzitumia vibaya ni lazima tutamtumbua tu! Tumeshawapa maelekezo Wakurugenzi wa Halmashauri pamoja na Maafisa Elimu wao na kuwaonya kuhusu matumizi ya fedha hizo,” alisema.

“Hatuhitaji mwanafunzi achangishwe hela ya mitihani, na zile shilingi 10,000/- kwa ajili ya wanafunzi wanaosoma Sekondari nazo pia tutazipeleka. Na huu ni mpango wa dharura ambao haukuwemo katika bajeti ya mwaka 2015/2016, kwa hiyo tutalazimika kuziombea kibali,” alisema.

Waziri Mkuu Majaliwa alisema Serikali imekwishafanya hesabu za kubaini kiasi kinachohitajika kwa ajili ya milo ya watoto shuleni kwa wale walioko bweni na wale wa kutwa. Hesabu tunazo na tumebaini kuwa tutazimudu,” alisema huku akishangiliwa.

“Serikali ilitoa ahadi kwa wananchi na sisi tumedhamiria kuzitekeleza. Tuliahidi elimu bure nasi tutaitekeleza,” alisema.

Naye Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo, Bw. Nape Nnauye amewataka madiwani wa jimbo la Ruangwa kuhakikisha wanamsaidia Waziri Mkuu Majaliwa kusimamia kazi za jimboni ili aweze kuwa huru kutekeleza majukumu ya kitaifa.

“Madiwani wa jimbo hili msaidieni Waziri Mkuu kusimamia shughuli za maendeleo ili wakati yeye anaendelea kutekeleza majukumu ya kitaifa, ya jimbo naye yawe shwari. Msaidieni kusimamia fedha za umma ziende kwenye miradi iliyokusudiwa ili wakati akitumbua majipu huko kwingine na huku pia yasiote,” aliongeza.