Jumatatu , 16th Mar , 2015

SERIKALI ya Tanzania imesaini mkataba wa ukarabati wa Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa (KIA) wa majengo na uwanja huo na kampuni ya ujenzi ya kimataifa ya Uholanzi iliyoshinda tenda ya kufanya kazi hiyo ndani ya miezi 23.

Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa (KIA).

Mkataba huo umesainiwa mwishoni mwa wiki na Meneja wa kampuni hiyo, Erick Van Zuthem na mwenzake Harko Kloeze ambaye ni mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo Afrika na Afrika ya Kati.

Upande wa Tanzania mkataba huo umesainiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa CADCO na Mhandisi Christopher Mkoma ambaye ni Mkurugenzi wa Uendeshaji na ufundi wa uwanja huo.

Akizungumza mara baada ya kusainiwa kwa mkataba huo, Mkurugenzi wa uendeshaji na ufundi wa uwanja huo, Mhandisi Christopher Mkoma amesema kuwa, wanatarajia kutumia Euro milioni 37 ambazo sawa na fedha za kitanzania zaidi ya shilingi bilioni 70.

Amesema katika ukarabati huo ulioanza mara moja baada ya kusaini mkataba huo watahakikisha unafanyika kwa wakati uliopangwa na bila kuharibu safari za Ndege.

Mkoma amesema Uwanja huo ulijengwa na Mwalimu tangu mwaka 1971 tangu wakati huo hadi leo haujawahi kukarabatiwa tena, hivyo uahitaji matengenezo makubwa ambayo yaatakwenda sambamba na kuongeza miundo mbinu ya maji safi na salama ili yaweze kuwa ya uhakika na mengi kulingana na mahitaji ya uwanja huo-

Amesema maji yanahitajika sana kwa sababu mbalimbali ikiwemo na kuhakikisha magari ya zimamoto hayakosi maji kwa usalama na ndege zinazotua na kuruka hapo.

Amesema kwa siku ndege 12 za kimataifa zinatua mbali na ndege za kawaida, hivyo ni vema uwanja huo ukaboreshwa zaidi ili kuvutia uwekezaji na wageni wengi.

Fedha hizo zimetolewa na serikali ya Tanzania na serikali ya Uholanzi, ili kuufanya uwanja huo unakuwa wa kisasa zaidi ya sasa.