Jumanne , 19th Sep , 2017

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Alhaji Abdallah Bulembo amewasilisha barua kwa Katibu Mkuu wa CCM kutogombea nafasi ya uenyekiti wa jumuiya hiyo kwa madai kuwa anaamini kati ya wagombea 48 waliojitokeza wanatosha. 

Mwenyekiti huyo wa jumuiya ya wazazi CCM amesema hatogombea tena nafasi hiyo na amewasilisha barua kwa Katibu Mkuu wa CCM kutogombea nafasi ya uenyekiti wa jumuiya hiyo na kueleza kuwa awali alichukua fomu kutokana na shinikizo kutoka kwa makatibu wakuu na wazee wa jumuiya hiyo.

"Leo nimewaita kuwaeleza sitagombea tena licha ya kuchukua fomu, naamini wagombea 48 waliopatikana, kuna mmoja atatufaa kuongoza jumuiya hii, leo ninapeleka barua kwa Katibu Mkuu wa chama ya kumweleza dhamira yangu hii,” amesema Bulembo 

Bulembo amesema uchaguzi katika ngazi ya Taifa utafanyika kuanzia Novemba 20 hadi 23, wagombea wote wapo lakini yeyote aliyeanza kampeni mapema huyo atakuwa ameshajiondoa mwenyewe.  

Kuhusu hoja ya kuchukua fomu amesema haikuwa dhambi kwa kuwa kanuni za chama zinaruhusu na upo uwezekano wa kuwa na nafasi mbili za uongozi.

"Kumekuwa na upotoshaji kwamba, ukiwa mbunge au waziri hauwezi kugombea nafasi nyingine,  hapa nina kitabu cha kanuni za mwaka 2005, 2010, 2012 na 2017 zinasema kiongozi au mbunge, waziri anaweza kugombea lakini kamati kuu ya chama itaamua inavyofaa, kama bado anahitajika atapitishwa lakini kwa upande wangu sitagombea" amesema.