Jumanne , 3rd Nov , 2015

Chama cha wananchi CUF kimesema kuwa kitakwenda mahakamani kupinga matokeo ya uchaguzi wa wabunge wa majimbo sita ambayo wanadai taratibu za uchaguzi zilikiukwa.

Mgombea Urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa(kulia) akimnadi Mgombea Ubunge Jimbo la Tabora Mjini kwa tiketi ya CUF, Peter Mkufya

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam mgombea ubunge wa jimbo la Tabora mjini Peter Mkufya amesema kuna taratibu nyingi zilikiukwa sana hasa wakati wa kuhesabu na kufanya majumuisho ambapo idadi ha kura zilizidi idadi ya walioandikishwa toka watu 138,000 hadi 140,000.

Mkufya ameongeza kuwa kulikuwa na vituo hewa vingi na hata walipoomba fomu ya malalamiko kwa mkurugenzi Wa uchaguzi walinyimwa na kudai kuwa siku ya majumuisho saa nane usiku katibu Wa CCM Wa wilaya ya Tabora mjini aliingia kwenye chumbani cha majumuisho kinyume na utaratibu.

Kwa upande wake afisa sheria na haki za binadamu Wa CUF Mohamed Mluya amesema wana ushahidi wa majimbo sita ambayo ni Newala, Pangani, Mtwara vijijini, Mbagala, Lindi Mjini na Tabora kwamba walishinda ila wameporwa ushindi na hivyo wataenda kudai ushindi wao mahakamani.