Jumanne , 14th Apr , 2015

Chama cha wananchi CUF kimesema kitendo cha kuahirishwa kwa kura ya maoni ni ubadhirifu wa pesa na muda wa Watanzani  unaotokana na serikali kudharau ushauri uliotolewa na vyama vya upinzani kuhusu mchakato wa katiba mpya.

Mwenyekiti wa CUF profesa Ibrahim Lipumba, amesema hayo jijini Dar es Salaam leo, katika hotuba yake kwa wajumbe wa mkutano wa baraza la uongozi la chama hicho, wanaokutana kujadili mambo mbali mbali ikiwemo mwenendo wa kisiasa nchini hivi sasa na jinsi chama hicho kilivyojipanga kudumisha ushirika wake na vyama vyote vinavyounda umoja wa katiba ya wananchi - UKAWA.

Kwa mujibu wa Profesa Lipumba, serikali imechukua muda mrefu kuto maamuzi ya kusitisha zoezi la kura ya maoni, hatua aliyodai ilifaa
kuchukuliwa mapema ili kunusuru mabilioni ya fedha za walipa kodi yaliyopotea kwa njia ambazo hazina maslahi kwa taifa.

Kauli ya Lipumba imekuja takribani wiki mbili baada ya tume ya taifa ya uchaguzi NEC kuahirisha zoezi la kura ya maoni iliyokuwa ifanyike mwishoni mwa mwezi huu, kutokana na kutokamilika kwa uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kwa mfumo wa BVR.