Alhamisi , 18th Apr , 2024

Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Kemirembe Lwota amepiga marufuku wakulima wa Tumbaku Wilayani humo kuwatumikisha watoto, wanafunzi na walio chini ya miaka 18 kwa kuwaajiri ili wawasaidie katika kazi zao mashambani.

Kemirembe Lwota Mkuu wa Wilaya ya Manyoni

DC Kemirembe ametoa marufuku hiyo wakati akizungumza na viongozi wa vyama vya Msingi katika AMCOS kwenye mkutano mkuu wa 26 wa mwaka wa chama kikuu cha Kilimo Ushirika na Masoko kanda ya kati Manyoni (CEAMCU) ambapo amesema kuwa tabia hiyo iachwe mara moja kwani kumtumikisha mtoto ni kosa kwa Mujibu wa Sheria za Nchi.

"Ndugu kama haya yanafanyika hapa kwetu naomba tuyaache mtakamatwa mtafungwa, wote tunajua kabisa kutumikisha watoto ni makosa na haipaswi na ni kinyume cha sheria ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania." Kemirembe Lwota, Mkuu wa Wilaya Manyoni

Hata hivyo amewataka wakulima wa Tumbaku kutumia matumizi bora ya majiko ambayo hayatumii kuni nyingi, badala ya kutumia nyingi kwa kuharibu mazingira bila kupanda miti mingine jambo ambalo linaharibu uoto wa asili na kisababisha jangwa.

"Kwenye maeneo mengi ya Tumbaku tumeona ukatakaji wa miti mkubwa sana kwa ajili ya Mabani, lakini huko nyuma nilisema kuna matumizi bora ya majiko ambayo hayatumii kuni nyingi haya mazingira tusipoyatunza huko mbele hata hiki kilimo tutashindwa kufanya, kwahiyo ni muhimu sana tutunze mazingira ni pia muhimu tupande miti mingi." alisisitiza DC Kemirembe Lwota