Ijumaa , 18th Aug , 2017

Naibu waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla anatarajia kuvishusha hadhi vituo vya afya sita vya jiji la Arusha na kuwa Zahati baada ya kubaini mapungufu makubwa waliyonayo.

Naibu waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla akiwa pamoja na wahudumu wa kituo cha Afya.

Dkt. Kigwangalla ametoa azimio hilo wakati alipokuwa kwenye ziara yake ya kikazi katika mkoa wa Arusha  na kutembelea katika vituo vya afya vikiwemo kituo cha Afya Kaloleni, Levolosi,  Ngarenaro, Daraja Mbili, Muriet mpya pamoja na kituo cha afya Mkonoo. 

"Ukaguzi wetu wa huduma za afya Arusha Jiji umebaini kuwa kati ya 'health centers saba' zilizopo, sita zinapaswa kushushwa hadhi kuwa zahanati", alisema Dkt. Kigwangalla.

Pamoja na hayo, Dkt. Kigwangalla amesema Wizara yake imedhamiria kuongeza ubora wa kutoa huduma na vipimo  kuanzia vituo vya Afya mpaka Zahanati.

"Tumedhamiria kuongeza ubora wa 'diagnosis' zote zinazofanywa mpaka ngazi ya kituo cha afya kwa kuhakikisha maabara zetu zinafanya kazi yake", alisitiza Dkt. Kigwangalla.

Katika hatua nyingine, Dkt. Kigwangalla ameagiza jengo la chumba cha upasuaji cha kituo cha Afya Daraja Mbili kianze kazi mara moja ndani ya wiki mbili na upasuaji ufanyike ikiwemo wataalamu kuwepo hapo muda wote.

"Nawaagiza ndani ya wiki mbili. Huduma za upasuaji zifanyike hapa kwani mnakila kitu, vifaa vingi na vya kutosha  na jengo zuri la kisasa", alisisitiza Dkt. Kigwangalla.

Kwa upande mwingine, Dkt. Kigwangalla amekiagiza kituo cha Afya Kaloleni kuhakikisha wanajenga wodi ya akina mama na kukamilisha maboresho ya chumba cha upasuaji.