Jumanne , 22nd Sep , 2020

Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe, amesema kuwa wakati anaendelea na kampeni zake mkoani Mtwara alifuatwa na mwanamke mmoja ambaye alimuuliza kama hawaoni haja ya wao kusimamisha mgombea mmoja, kitendo ambacho anadai kilimpa uchungu.

Zitto Kabwe.

Zitto ameyaandika hayo hii leo Septemba 22, 2020, kupitia ukurasa wake wa mtandao wa twitter,na kuongeza kuwa kitendo hicho kilimfikirisha na kuona kwamba Watanzania wanayo kiu ya kupata mabadiliko.

"Nimezunguka nchi yetu na kuona hisia za Watanzania, juzi Mtwara Mjini alinifuata mama mtu mzima sana na kuniambia “mwanangu mmeshindwa kukubaliana mgombea mmoja?, tafadhali mwanangu jitahidini”, nilipata uchungu sana moyoni, Watanzania wanataka mabadiliko tunawapa", ameandika Zitto Kabwe.

Ikumbukwe kuwa awali chama hicho kilimsimamisha Bernard Membe, aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na mwanachama wa CCM, ambaye alihamia ndani ya chama hicho baada ya kufukuzwa uanachama na chama chake cha awali kuwa mgombea wa urais kupitia chama hicho, na siku ya jana Septemba 21, 2020, ACT Wazalendo walitangaza kumuunga mkono Tundu Lissu.