Jumatatu , 14th Oct , 2019

Mwanasheria mbobezi na wakili, Fatma Karume ametaja kitu kikubwa anachokipenda na kukikumbuka kutoka kwa hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Fatma Karume

Ameyasema hayo pindi alipotembelewa ofisini kwake na Big Chawa wa Planet Bongo ya East Africa Radio, ambapo amesema kuwa anaikumbuka picha ambayo ipo ofisini kwake ikimuonesha babu yake, Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume, Mwl. Julius Kambarage Nyerere na aliyekuwa kiongozi wa Ethiopia, Haile Selassie.

Amesema anakumbuka mengi anapoiona picha hiyo, hasa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwani kipindi babu yake ambaye alikuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume amefariki, Mwl. Nyerere ndiye alikuwa ni kama babu yake aliyebakia.

"Naipenda sana picha hii (akiionesha) hapa ofisini kwangu, ninampenda sana babu yangu na huyu mbwa wa Haile Selassie hapa, lakini pia nampenda sana mwalimu kwa sababu pia alipofariki babu yangu, yeye alikuwa babu yangu aliyesalia", amesema Fatma huku akionesha picha hiyo.

Leo ni kumbukumbu ya miaka 20 tangu kifo cha Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere kilichotokea, Oktoba 14, 1999.