Jumatatu , 3rd Jun , 2019

Spika wa Bunge Job Ndugai amezuia kusomwa kwa hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, kwa Wizara ya Fedha iliyokuwa isomwe na Mbunge wa Momba, David Silinde kwa kile Spika alichokidai kuwa ina maneno yasiyokuwa na maadili, inayodaiwa kuandaliwa na Mbunge, Halima Mdee.

Spika wa Bunge Ndugai ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma wakati wa mjadala wa hoja ya Wizara ya Fedha ambapo upande wa Kambi Rasmi ya Upinzani ulipaswa kuwasilisha maoni yao.

Spika Ndugai amesema kuwa, "hapa tunatoka sisi lakini vizazi vyetu vinakuja, na watasoma hivi vitabu, haiwezekani mtu umesimamishwa halafu unashiriki kufanya kazi za Bunge", amesema Ndugai.

Halima Mdee kwa sasa anatumikia adhabu ya kusimamishwa vikao vya Bunge kufuatia kuhukumiwa juu ya maamuzi yake ya kuunga mkono kauli ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali kuwa Bunge ni dhaifu.