Jumatatu , 3rd Feb , 2020

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa William Anangisye, amesema kuwa muda wowote kuanzia sasa wataweza kuwaita viongozi Sita wa Serikali ya wanafunzi wa chuo hicho (DARUSO), waliosimamishwa masomo kwa ajili ya hatua zingine.

DARUSO , kulia ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa William Anangisye.

Akizungumza na EATV&EA Radio Digital leo Februari 3,2020 Profesa Anangisye amesema kuwa uchunguzi wa awali waliokuwa wanaufanya dhidi yao umekwishakamilika kwa kiasi fulani na kwamba wataweza kuwaita mara baada ya taratibu zao kukamilika.

"Tuko kwenye mchakato wa kuwaita na ile barua ilikuwa inasema pending investigation sasa hivi tumeshamaliza na tumefikia kwenye hatua fulani, na suala la masomo lina taratibu zake na nadhani hadi keshokutwa (Jumatano Februari 5) nitakuwa na nafasi nzuri ya kuliongelea" amesema Profesa Anangisye.

Viongozi Sita wa DARUSO akiwemo Rais wao walisimamishwa masomo Disemba 18, 2019 na uongozi wa chuo baada ya kupokea maagizo kutoka kwa Waziri wa Elimu Profesa Joyce Ndalichako, aliyetoa masaa 24 kwa uongozi wa chuo kuwachukulia hatua stahiki baada ya DARUSO kutoa tamko la masaa 72 kwa Bodi ya Mikopo, wakishinikiza kulipwa madai yao ya mikopo.