Jumatatu , 13th Apr , 2015

Kutokana na Changamoto zinazoikabili Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga ya Bombo Klabu ya Rotary Kupitia tawi lake la mkoa wa Tanga imepeleka kiasi cha shilingi millioni 18 za kitanzania kwaajili ya kuboresha Huduma za Uzazi, Mama na Mtoto.

Hayo yamesemwa na Rais wa Rotary Klabu Tanga Dkt, Wiliam Mwengee wakati akizungumza na East Africa Radio kuhusiana na changamoto zinazoikabili Hospitali hiyo na kuona kuwa ipo haja ya kusaidia baadhi ya changamoto zilizo ndani ya uwezo wao.

Dkt. Mwengee ambaye ni mmoja kati ya wajumbe wa bodi katika Hospitali hiyo amesema kutokana na kutanuka kwa sekta ya afya hivyo kunahitajika kuongezewa vifaa mbalimbali vya kutolea huduma katika Hospitali hiyo.

Dkt, Mwengee ameongeza kuwa mara baada ya klabu hiyo kupata fedha hizo wameona ni vyema zikasaidia katika wodi ya kina mama ili kuboresha huduma za uzazi pamoja na mtoto katika Hospitali hiyo.

Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga ya Bombo inahudumia asilimia kubwa ya wakazi waishio mkoani humo hivyo ni vyema serikali na mashirika binafsi kuguswa katika kujitolea misaada mbalimbali ili huduma za Hospitali hiyo zizidi kukua.