Jumanne , 29th Mar , 2016

Kamati ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji imeitaka Mamlaka ya Bandari nchini—TPA kurekebisha mwenendo wake wa matumizi ya pesa sambamba na kuwa na mipango inayotekelezeka ya kuongeza ufanisi tofauti na ilivyokuwa miezi michache iliyopita.

Mbunge wa Mtwara Mjini Bw. Maftah Abdallah Nachuma

Wajumbe wa Kamati hiyo, mbunge wa Mbeya Vijijini Bw. Oran Njeza pamoja na mwenzake wa Tunduma wamesema taarifa ya fedha ya mamlaka hiyo inaonesha uwepo wa mapungufu makubwa ambayo yasiporekebishwa, mchango wa sekta ya bandari katika uchumi utaendelea kudidimia siku hadi siku.

Aidha, mbunge wa Mtwara Mjini Bw. Maftah Abdallah Nachuma amehoji, dhana ya mradi wa ujenzi wa bandari mpya ya Bagamoyo, wakati ambapo mamlaka hiyo imekuwa ikihaha kutafuta pesa kwa ajili ya kuboresha bandari zake ikiwemo ya Mtwara ambayo inahitaji ukarabati mkubwa chini ya mradi wa ukanda wa kiuchumi wa Mtwara.

Kwa upande wake, Mbunge wa Bunda Mjini Bi. Easter Bulaya amehoji ni kwanini TPA imekuwa haishughulikii tatizo la bandari bubu zilizozagaa maeneo mengi ya ukanda wa bahari ya Hindi, hasa katika mikoa ya Pwani na Dar es Salaam, huku mizigo inayopitia katika bandari ya Dar es Salaam ikiwa inapungua.