Jumatatu , 21st Jan , 2019

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali CAG Prof. Musa Assad leo amehojiwa kwa zaidi ya saa tatu naKamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka, kutokana na kauli yake ya kuliambia bunge ni dhaifu wakati akihojiwa na redio moja nchini Marekani hivi karibuni.

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali CAG Prof. Musa Assad akiwa kwenye Kamati ya Maadili leo asubuhi.

Saa tano kamili asubuhi akisindikizwa na maafisa wa bunge Pof. Assad ameingia bungeni kisha kujiandikisha katika kitabu cha wageni kabla ya kuingia ukumbi wa mahojiano saa 5 na dakika sita ambako alihojiwa hadi saa 8:47 mchana.

Akizungumza na wanahabari baada ya mahojiano ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka, Mwenyekiti wa Kamati hiyo,Mbunge wa Tabora Mjini, Emmanuel Mwakasaka amekiri kwamba CAG amehudhuria mahojiano na kutoa ushirikiano mkubwa hivyo mapendekezo yatapelekwa kwa spika Job Ndugai.

“Ametoa ushirikiano wa kutosha na amejibu maswali yote ambayo alikuwa anaulizwa na wajumbe. Shahidi Profesa Assad ametoa ushirikiano wa kutosha. Ametusaidia kwa kila hatua tuliyofikia na kila swali aliloulizwa amejibu, tunamshukuru sana,” alisema Mwakasaka.

Kikao hicho kilihusisha karibu wajumbe wote 18 wa Kamati.

Januari 7, 2019 Spika Job Ndugai alimtaka CAG kufika Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuhojiwa kutokana na kauli yake ya aliyoisema akiwa nje ya nchi kwa kusema kuwa  bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni dhaifu.