Alhamisi , 18th Jul , 2019

Mkurugenzi wa mashtaka nchini Biswalo Mganga, amefuta kesi 75 zinazowakabili mahabusu na wafungwa mbalimbali katika gereza kuu la Butimba mkoani Mwanza na kuwataka wahusika kutorudia makosa.

Miongoni mwa askari 8 walioachiwa huru pamoja na mahabusu wengine.

Miongoni mwa kesi zilizofutwa ikiwemo kesi namba moja ya uhujumu uchumi ya mwaka 2019, iliyokuwa ikiwakabili askari polisi nane waliohusika na utoroshaji wa madini  kilo 319 yenye thamani ya shilingi bilioni 27.

Hatua hiyo imekuja siku moja baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. John Pombe Magufuli, kutembelea gereza kuu la Butimba na kuzungumza na wafungwa pamoja na Mahabusu.

Wakizungumza na waandishi wa habari Waziri wa katiba na sheria Balozi Agustino  Mahiga pamoja na mkurugenzi wa Mashtaka nchini DPP Biswalo Mganga mara baada ya kufanya ziara katika gereza hilo na kuzungumza na wafungwa na Mahabusu kwa zaidi ya saa 7, wamebaini baadhi ya waliomo katika gereza hilo wamebambikiwa kesi.

''Wapo waliobambikiziwa kesi lakini sio mahabusu wote waliopo gerezani hapo wamebambikiziwa wengine ni kweli wahusika wa kesi, niwaombe tu waendapo uraiani hali ikaendelee kuwa shwari kama ilivyokuwa wakati wakiwa gerezani'', amesema Biswalo.

Katika ziara iliyofanywa na Waziri wa katiba na sheria na Balozi Agustino  Mahiga pamoja na mkurugenzi wa Mashtaka nchini DPP Biswalo Mganga wametembelea magereza mbalimbali ya mikoa ya kanda ziwa na kufuta jumla ya kesi 325.