Alhamisi , 29th Nov , 2018

Mahakama ya Rufani nchini, leo imesikiliza kesi ya Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA, Freeman Mbowe, na Mbunge wa Tarime Mjini Esther Matiko juu ya hatma ya kufutiwa ama kutofutiwa dhamana yao.

Mbunge wa Tarime Mjini Esther Matiko, na Freeman Mbowe Mwenekiti wa CHADEMA Taifa.

Shauri hilo la Mahakama liliwasilishwa jana na Wakili upande wa utetezi anayemtetea mtuhumiwa Freeman Mbowe na Matiko ambapo kupitia Jaji Rumanyika, Mahakama hiyo iliagiza kesi hiyo kusikilizwa leo saa 2 asubuhi.

Leo hii mahakamani hapo, upande wa mashtaka kupitia kwa wakili wa Serikali, Dkt Zainabu Mango aliwasilisha hoja tatu za kupinga kusikilizwa kwa rufaa hiyo kwa kile walichodai kukata rufaa si sahihi.

Sababu nyingine waliyoieleza kuwa kifungu walichokitumia hakitoi uhalali wa mahakama wa kusikiliza rufaa hiyo sambamba na kudai watuhumiwa  wamekuwa na mwenendo usioridhisha kwenye kesi ya msingi.

Kupitia hoja hizo za upande wa Jamhuri, Jaji wa mahakama ameahirisha kesi hiyo hadi kesho saa 5 kwa ajili ya kutoa ya mapingamizi ya Jamhuri.

Novemba 23 mwaka huu kupitia mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu iliwaondolea dhamana, Freeman Mbowe na Esther Matiko, baada ya kukiuka masharti ya dhamana.