Jumatano , 16th Sep , 2020

Mgombea Urais kupitia CCM Dkt John Magufuli amesema kuwa alizunguka nchi nzima kutafuta mtu ambaye anafaa kuwa Katibu Mkuu wa CCM na ndipo alipokutana na Dkt Bashiru Ally kwa kuwa ni miongoni mwa wazalendo wachavche wanaofuta miiko ya Baba wa Taifa.

Kushoto ni mgombea Urais Dkt John Magufuli na kulia ni Katibu Mkuu wa CCM Dkt Bashiru Ally.

Dkt Magufuli ametoa kauli hiyo hii leo Septemba 16, 2020, katika mkutano wake wa kampeni alipokuwa akiomba kura kwa wananchi Bukoba mkoani Kagera, na kuongeza kuwa lengo la yeye kuzunguka nchi nzima ilikuwa ni kuhakikisha anapata Katibu Mkuu ambaye ni mzalendo wa kweli.

"Dkt Bashiru huyu ni mtu ambaye ametoka katika maisha ya chini, amefanya biashara ya kuuza Ndizi pale Kemondo na nafikiri alipata na mke hapo hapo, lakini ni mzalendo kati ya wazalendo wachache wenye kufuata miiko ya Baba wa Taifa, kwenye chama hiki niliona nahitaji mtu namna hiyo, na ndiyo maana nikamteua awe Katibu Mkuu wa CCM", amesema Dkt Magufuli.

Awali akizungumzia suala la moto ulioteketeza bweni la shule ya Byamungu Islamic akatoa maagizo haya, "Kutokana na msiba uliotupata nazihimiza mamlaka zote husika TAMISEMI na Wizara ya Elimu kuhakikisha shule zote zinazingatia masuala ya usalama kabla na baada ya kuanzishwa ili madhara ya moto katika shule zetu yasijirudie tena".