Jumapili , 6th Mar , 2016

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein, kufuatia kifo cha mmoja wa waasisi wa Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar Mzee Hamid Amer.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli.

Marehemu Mzee Hamid Amer jana mchana mjini Unguja, akiwa ni miongozi mwa wanamapinduzi vinara waliopigania kuondolewa kwa utawala wa kisultani huko Zanzibar.

Katika uhai wake marehemu amewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi, zikiwemo uwaziri na ujumbe wa Baraza la Wawakilishi.
Rais Magufuli ameelezea kushtushwa na kifo cha Mzee Hamid Amer na amesema Taifa limempoteza mtu muhimu aliyejitoa muhanga kupigania Uhuru, Haki na Maslai ya wananchi.

"Nakupa pole nyingi Mheshimiwa Rais Shein kwa msiba mkubwa ulioikumba Zanzibar na kupitia kwako napenda kuwapa pole nyingi familia ya Marehemu, Ndugu, Jamaa na Marafiki wote." Amesema Rais Magufuli.

Dkt. Magufuli ameongeza kuwa anaungana na Wazanzibari wote kuomboleza kifo cha shujaa huyo na mwanamapinduzi wa kweli, na amewataka wote walioguswa na msiba huo kuwa na subra.

Marehemu Hamid Amer anakuwa mwanapinduzi wa 11 kufariki dunia kati ya wanamapinduzi 12 waliokuwa mstari wa mbele kuongoza mapambano ya kuung'oa utawala wa kisultani huko Tanzania Zanzibar.

Rais Magufuli amemuomba Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya Marehemu Hamid Amer mahali pema peponi, Amina