Jumatatu , 4th Dec , 2023

Jumla ya watu 63 wamefariki dunia na wengine 116 wamejeruhiwa kufuatia maporomoko ya matope yaliyotokea wilayani Hanang’ mkoa wa Manyara.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, wakati akiaga miili ya waliofariki kutokana na maporomoko ya tope mkoani Manayara

Taarifa hiyo imetolewa leo Desemba 4, 2023, na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, wakati wa zoezi la kuaga na kuikabidhi miili hiyo kwa ndugu zoezi lililofanyika katika viwanja vya shule ya msingi Katesh.

"Leo nikiwa mbele yenu na sisi sote tukiwa mbele ya ndugu zetu 63 kati yao wanaume ni 23, wanawake ni 40, kati ya hawa, watu wazima kuanzia 18 kwenda juu wanaume ni 14 na wanawake ni 26 na watoto wadogo chini ya miaka 18 wanaume ni 9 na wanawake ni 14 hawa wote ndio ambao wamelala mbele yetu," amesema Waziri Mkuu

Aidha Waziri Mkuu ameongeza kuwa, "Kwenye madhara haya tumepata majeruhi pia wapatao 116, wanaume ni 56 na wanawake ni 60, ndugu Watanzania haya maafa ni makubwa sana, baada ya kuwa tumeeleza idadi ya vifo na majeruhi lakini pia tumepata uharibifu mkubwa wa nyumba za kuishi, mashamba na mitambo mbalimbali ya magari, nimepata bahati ya kwenda Gendabi nyuma ya milima, kile kijiji nyumba zimeachwa upande wa kulia na kushoto eneo la katikati nyumba zote zimeondoka limebaki kanisa tu, hali sio nzuri,".

Aidha zoezi la kutafuta miili ya watu wengine kwenye tope linaendelea