Jumanne , 10th Dec , 2019

Mfungwa mmoja aliyejulikana kwa jina la Merald Abraham, amekataa kurejea Uraiani baada ya kuachiwa kwa msamaha uliotolewa na Rais Magufuli kwa madai ya kuwa hana pa kwenda na kutaka ahamishiwe katika Gereza la Ukonga, Jijini Dar es Salaam.

Mfungwa Merald Abraham, aliyekataa kurudi Uraiani

Abraham ni miongoni mwa wafungwa 70 katika Gereza la Ruanda, waliopewa msamaha jana Desemba 9, 2019, na leo Desemba 10 wakati wenzake wakiachiwa huru, yeye alikataa kubaki huru hali iliyopelekea kujijeruhi usoni, akishinikiza kuendelea kubaki mahabusu.

"Sina pa kwenda, bora nibaki Gerezani, ikiwezekana nitolewe hapa nihamishiwe Gereza la Ukonga Dar es Salaam, ila sio Uraiani" amesema Abraham.

Jana wakati wa Maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanzania, ambayo Kitaifa yalifanyika mkoani Mwanza, Rais Magufuli alitoa msamaha kwa wafungwa takribani 5,533 na wafungwa 259 kati yao wanatoka mkoani Mbeya.