Alhamisi , 8th Oct , 2015

Mgombea ubunge jimbo la Mtwara mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Joel Nanauka, aliyedaiwa kutoweka katika mazingira ya kutatanisha hatimaye ameonekana katika zahanati ya Bursa iliyopo manispaa ya Mtwara akipata matibabu.

Mgombea ubunge jimbo la Mtwara mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Joel Nanauka,

Akizungumza na waandishi wa habari, daktari wa Zahanati hiyo aliyempokea na kushughulika na huduma ya kwanza kwa mgombea huyo kabla ya kumpatia rufaa ya kwenda hospitali ya mkoa ya Ligula, Dkt. Pendo Mmbando, amesema alipokelewa hospitalini hapo alfajili ya jana akiwa mwenyewe bila ya kuambatana na mtu.

Kwa upande wake, mganga mfawidhi wa hospitali ya Ligula, Dkt. Mdowe Mhuza, amesema kwa mujibu wa maelezo yake ni kwamba aliokotwa mahali ambapo alihisi kuwa alipewa dawa za usingizi na baadae kupelekwa katika zahanati hiyo kabla ya kufikishwa hospitalini hapo ambako alifanyiwa uchunguzi ambao hata hivyo hawakubaini kuwa na majeraha yeyote mwilini mwake.

Aidha, baba mzazi wa mgombea huyo, mzee Grey Nanauka, hakutaka kulihusisha moja kwa moja tukio hilo na maswala ya kisiasa ukizingatia kuwepo kwa mvutano wa jimbo uliopo baina ya vyama vitatu kati ya vine vinavyowakilisha Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) vya NCCR-Mageuzi, CHADEMA na Chama cha Wananchi (CUF).

Kamanda wa polisi mkoa wa Mtwara, Henry Mwaibambe, amethibitisha kupokea taarifa za kupotea kwa mgombea huyo ambapo zilipokelewa ofisini kwake jana saa saba mchana zikidai kuwa aliaga nyumbani kwake kuwa anakwenda maeneo ya Mnarani kwa ajili ya kukutana na jamaa zake na hakuonekana tena baada ya hapo.