Jumatatu , 21st Jan , 2019

Mkuu wa mkoa wa Rukwa, Mh. Joachim Wangabo amewashauri wananchi wote wanaoharibu misitu kwa kuchoma moto kwaajili ya kuwinda panya waanze kufuga kuku ili kuweza kuokoa mazingira.

Mkuu wa mkoa wa Rukwa, Mh. Joachim Wangabo

Amesema hayo wakati akizungumza na Wakurugenzi wa Halmashauri za Mkoa huo, ambapo amewaagiza kuhakikisha kuwa halmashauri zao zinapanda miti milioni 1.5 ili kuzuia uharibifu unaotokana na shughuli hizo. 

Kwa hiyo naagiza Wakurugenzi wote wa Halmashauri zetu kuwasilisha mpango mkakati wa upandaji miti kwa kipindi cha Mwaka huu, ikiwa ni pamoja na kubainisha idadi ya miti waliyonayo na mahali ilipo pamoja na ya wadau wao wa utunzaji wa mazingira, na maeneo ya kupanda.  Mpango huu unifikie ndani ya siku tano kuanzia leo”, amesisitiza. 

Vile vile alizitaka Taasisi za Serikali kama shule, magereza na vyuo vya elimu kuanza kutumia nishati mbadala ikiwemo ya “biogas” katika shughuli zao za mapishi ya chakula na kupunguza kasi ya matumizi ya kuni kwani mkoa una mitambo 2 ya “biogas” katika Manispaa ya Sumbawanga katika Vijiji vya Mtimbwa na Ntendo ambayo inatumika kama darasa la kujifunzia  ujuzi wa kutengeneza biogas kutokana na mabaki ya mifugo yetu.

Maagizo hayo ya Mkuu wa Mkoa yalikujaa baada ya Afisa Ardhi na Maliasili wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, Juma Chande kueleza katika msimu wa mwaka 2018/2019 katika kata 8 kati ya kata 27, halmashauri imeshapanda miti 292,899 ambayo ni asilimia 17.4 ya lengo na kufafanua kuwa halmashauri inaendelea kutoa elimu ya kutunza mazingira, kupanda miti na kilimo mseto huku akitaja changamoto zinazorudisha nyuma juhudi hizo, likiwemo suala hilo la uwindaji wa panya.

Miongoni mwa changamoto ni muitikio mdogo wa wananchi katika utunzaji wa mazingira pamoja na hamasa nyingi kutolewa kwao, mila na tamaduni za wananchi za uwindaji wa panya mathalani kusababisha uchomaji wa miti wakati wa kiangazi mfano maeneo ya vijiji vya Msandamuungano, Sandulula na Mpwapwa hivyo kuathiri misitu iliyopandwa”, aliongeza.

Bonyeza hapa chini kutazama zaidi.