Jumatano , 26th Jun , 2019

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Kenya imekanusha kauli iliyotolewa na Mbunge wa jimbo la Starehe nchini humo, Charles Njagua Kanyi maarufu Jaguar kuwa si kauli ya Serikali, hivyo amewataka Watanzania wawe watulivu.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo wakati akitoa kauli ya Serikali kuhusu kauli iliyotolewa na Mbunge huyo na kuwataka wafanyabiashara kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania waondoke nchini Kenya ndani ya saa 24.

Amesema baada ya Mbunge huyo kutoa kauli yake, Serikali ya Tanzania ilianza kulifanyia kazi jambo hilo ambapo ilimuita Balozi wa Kenya nchini Tanzania ili kujua kama huo ni msimamo wa Serikali yao ama la, ambapo balozi huyo alimesema ile si kauli ya Serikali ya Kenya wala ya wananchi.

Si kauli nzuri na kauli hii iliyotolewa na mtu mmoja inajenga chuki baina ya mtu na mtu, nchi na nchi na tayari Serikali ya Kenya inalifanyia kazi suala hili na imetuomba Watanzania tuendelee kuwa wavumilivu.”

Waziri Mkuu amesema tamko hilo linaweza kuibua chuki na vurugu miongoni mwa nchi mbalimbali zikiwemo za Afrika Mashariki na tayari Wabunge wa Bunge Afrika Mashariki wanaoendelea na kikao cha Bunge hilo jijini Arusha wamepinga na kulaani kauli hiyo.

Hivyo, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasihi Watanzania popote walipo waendelee kuishi vizuri na Wakenya kwa kuwa wao hawana chuki na Watanzania bali ni mtu binafsi. Pia amewatahadharisha wananchi wa Afrika Mashariki wawe makini na kauli zao ili kuepusha vurugu.