Alhamisi , 5th Nov , 2015

Rais Mteule Dkt. John Pombe Magufuli anaapishwa leo kuwa Rais wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi baada ya kushinda katika uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25 mwaka huu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akizungumza na rais mteule wa awamu ya tano Dkt. John Pombe Magufuli

Dkt. Magufuli alivuna asilimia 58.46 ya kura halali zilizopigwa na kuwazidi wagombea wengine saba akiwemo Mpinzani wake mkuu katika kinyang'anyiro hicho waziri mkuu wa Zamani Mh. Edward Ngoyai Lowassa.

Jana Rais Kikwete anayemaliza muda wake wa awamu ya nne alitangaza mapumziko ya kitaifa hii leo kupisha tukio hilo kubwa na la Kihistoria la kuapishwa mrithi wake katika serikali ya awamu ya tano Dkt. John Magufuli.

Viongozi mbalimbali wa kitaifa na kimataifa wanatarajiwa kuhudhiria katika shughuli hiyo wakiwemo marais saba kutoka nchi mbalimbali wakiwemo marais wote wa Afrika Mashariki pamoja Rais wa Afrika kusini Jacob Zuma.

Hapo jana Baraza la wazee jijini Dar es Salaam walimtaka Rais huyo mteule anayeapishwa leo kuwaunganisha watanzania na kutumia busara katika uongozi wake huku akiwataka walioshindwa katika kinyang'anyiro hicho kuungana katika kuleta maendeleo na amani ya nchi.