Jumatano , 16th Sep , 2015

Wakazi wa halmashauri ya mji wa Nanyamba mkoani Mtwara wamelalamikia tatizo la uhaba wa maji lililodumu kwa miaka mingi kiasi cha kulazimika kusafiri umbali wa kilomita zaidi ya 50 mpaka Ruvuma kufuata huduma hiyo.

Aliekua Mwenyekiti wa Kamati Ndogo ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Amina Makilagi akipanda ngazi za tanki la maji la mradi wa Maji wa Nanyamba.

Wakizungumza na East Africa Radio, baadhi ya wananchi hao walisema maji wanayotumia sio salama kwasababu ni ya mabwawa ambapo hata hivyo upatikanaji wake wanalazimika kusafiri kwa zaidi ya kilomita 10, hali inayopelekea kuzorotesha shughuli zingine za kimaendeleo.

Aidha, mgombea ubunge wa jimbo la Nanyamba kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Abdallah Chikota, ambaye amekosa mpinzani katika jimbo hilo ameahidi kutatua tatizo hilo, kwa kufufua na kuanzisha miradi mingine ya maji.

Kwa upande wake, mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Oscar Ng’itu, amesema zipo baadhi ya changamoto ambazo zinapelekea uwepo wa tatizo hilo ikiwa ni pamoja na kukosa nishati ya uhakika katika vyanzo vya maji na kulazimika kutumia mafuta kiasi cha zaidi ya lita 150 kwa siku kwa ajili ya kuwasha jenereta, ambalo haliwezi kufanya kazi kwa saa 24.