Alhamisi , 14th Mar , 2019

Spika wa Bunge Job Ndugai amesema hajapata taarifa yeyote juu ya kuzuiliwa kwa mshahara wa Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu, huku akimtaka Mbunge huyo kuandika barua kwa ofisi ya Spika juu ya madai yake.

Spika wa Bunge Job Ndugai .

Spika Ndugai ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na www.eatv.tv iliyotaka kufahamu juu ya kauli yake dhidi ya madai ya Mbunge Tundu Lissu ambaye amelalamikia kusitishwa kwa mshahara wake.

Ndugai amesema "kiukweli sijasikia lolote lakini hayo madai ya mshahara alimwandikia Spika barua kwamba hakupata mshahara wake na akajibiwa ni kwanini hakupewa mshahara wake".

"Bunge linataratibu kwani hata wewe ukiwa hujapata mshahara huwa unadai kwenye mitandao, hebu muulize kwanza yeye amezifuata hizo taratibu?" ameongeza Ndugai.

"Unajua nyinyi mnawafanya wabunge kama Mungu watu ila wabunge ni kama watumishi wengine wa umma kama wewe unavyokuwa hujapata mshahara Mbunge anatakiwa afanye hivyohivyo."

Mapema leo Machi 14, 2019, katika mitandao ya kijamii ameonekana Mbunge wa Singida Mashariki akilalamikia juu ya kuondolewa kwa mshahara wake.