Jumapili , 1st Nov , 2020

Tume ya Taifa ya Uchaguzi imesema kuwa tayari imeshatoa fomu kwa vyama vya siasa ili kupendekeza majina ya wabunge watakaopata nafasi ya kuwakilisha kupitia viti maalum na chama kitakachopata nafasi hiyo lazima kiwe na asilimia kuanzia 5% za kura za wabunge.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Dkt. Wilson Mahera.

Akizungumza wakati akitoa taarifa fupi ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 28, 2020, katika hafla ya kumkabidhi cheti mshindi wa kiti cha Urais, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume hiyo, Dkt. Wilson Mahera, amesema kuwa chama kitakachopata  angalau asilimia 5% ya kura za wabunge  kitakuwa na  uhalali wa kupata  wabunge wa viti maalum.

"Chama kitakachopata angalau asilimia 5% ya kura za wabunge kitakuwa na uhalali wa kupata wabunge wa viti maalum", amesema Dkt. Mahera.

Aidha ameongeza kuwa, "Tume ilitoa kibali cha utoaji wa elimu ya mpiga kura kwa asasi 245 kwa Tanzania bara na 7 visiwani Zanzibar. Tanzania inatumia mfumo  ambao mgombea anaepata kura nyingi zaidi  ndiye hutangazwa kuwa mshindi”.