Jumatano , 20th Mei , 2020

Mwanasheria wa msanii Idris Sultan, Ben Ishabakaki, amesema kuwa jana walishindwa kumtoa mteja wake Polisi, baada ya kunyimwa dhamana kwa kile walichoelezwa kuwa, hilo ni agizo kutoka Mamlaka za juu za Jeshi la Polisi.

Mchekeshaji, Idris Sultan.

Ishabakaki ameyabainisha hayo leo Mei 20, 2020, wakati akizungumza mubashara kwenye kipindi cha SupaBreakfast ya East Africa Radio, na kueleza kuwa hata baada ya kufika kituoni hapo aliambiwa Askari aliyemshikilia hana mamlaka ya kumhoji na kwamba anasubiri maagizo kutoka Makao Makuu ya Polisi.

"Tulimuombea dhamana lakini pale kituoni OysterBay wakasema hawana mamlaka mpaka tuongee na DCI, lakini DCI akatuambia hilo suala halijui, mpaka saa 2 usiku tulikosa dhamana, hivyo amelala mahabusu" amesema Ben Ishabakaki, Mwanasheria wa Idris Sultan.

Aidha Mwanasheria huyo ameeleza namna Idris alivyoripoti kituoni hapo, "Jana yeye alipigiwa simu na Meneja wake, alikuwa ameitwa amtafute Idris, kwahiyo alipofika pale kuna Inspekta mmoja anaitwa Noel wa kitengo cha makosa ya kimtandao, ndiyo alisema amepewa 'Order' ya kumshikilia kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi".