Rais Shein yupo nchini humo kwa ziara ya wiki moja iliyoanza Septemba 23, ambapo itafikia ukomo Septemba 28 na anatarajiwa kurudi nchini Septemba 29,2019.
Katika mazungumzo yao na mtawala huyo amemhakikishia kuwa yuko tayari kuisaidia Zanzibar katika kuimarisha sekta ya elimu kwa kuongeza ufaulu hasa kwa wanafunzi wanaosoma elimu ya juu.
Sheikh Saud Bin Saqr Al Qasimi amesema kuwa nchi yake imepiga hatua nzuri katika kuimarisha sekta ya elimu, hasa elimu ya juu na hivyo wapo tayari kutoa fursa kwa walimu wa Zanzibar kwenda nchini humo kujifunza katika vyuo vikuu vilivyopo.
Katika ziara hiyo pia Rais Shein, atakwenda Abu-Dhabi kwa ajili ya kushuhudia utiaji wa saini mkataba wa mashirikiano katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali hiyo kupitia mfuko wa Khalifa Fund wenye makao makuu yake nchini humo.

