Jumamosi , 26th Dec , 2020

Rais Dkt. Magufuli kupitia kwa RC Mbeya, Albert Chalamila, amekanusha uvumi wa taarifa zilizokuwa zikisambaa mitandaoni kwamba, serikali imepanga kuibomoa Hoteli ya aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kupitia CHADEMA Joseph Mbilinyi ambayo ilidaiwa kuwa imejengwa kwenye chanzo cha maji.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli.

Uamuzi huo wa Rais Dkt. Magufuli, umetolewa leo Desemba 26, 2020,  na mkuu wa mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila, ambaye alitembelea eneo la uwekezaji wa Hoteli hiyo na kusema kuwa eneo hilo linafaa na kuwaomba Watanzania hususani wanasiasa na wafanyabiashara, kuacha kusambaza chuki zinazoharibu biashara za mbunge huyo mstaafu.

"Nimetembelea Hoteli ya Sugu kwa lengo la kuangalia uwekezaji alioufanya, nimeridhika na ninampongeza aendelee kuwekeza zaidi, namtoa hofu Sugu kwamba Hoteli yake haitavunjwa kwa sababu amezingatia utaratibu wote wa uwekezaji, hoteli hii siyo ya chama fulani cha siasa na kila mtu bila kujali rangi wala kabila anakaribishwa kuwekeza mkoani Mbeya", amesema RC Chalamila.

Kwa upande wake mbunge mstaafu wa jimbo hilo Joseph Mbilinyi maarufu kama Sugu, amemshukuru Rais Dkt. Magufuli, kwa kauli hiyo na kwamba hakuwa na wasiwasi kwani alizingatia taratibu zote za uwekezaji na kwamba nyaraka za taasisi zilizotoa kibali alizihifadhi.