Alhamisi , 18th Oct , 2018

Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), anayetambulika na msajili wa vyama vya siasa nchini, ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Kaliua, Magdalena Sakaya amesema kuwa hawezi kuhama CUF kwa sababu yoyote ile na hawezi kununuliwa kwakuwa hana bei.

Magdalena Sakaya

Sakaya amesema kuwa anafanya kazi kwa misimamo aliyojiwekea na hawezi kutetereka katika nafasi yake, kwani kwa kufanya hivyo atakuwa hawatendei haki wananchi wake waliompigia kura mwaka 2015.

Sakaya ametoa kauli hiyo leo Oktoba 18, katika mahojiano maalum na www.eatv.tv, ambapo amesema kuwa anaunga juhudi za Rais akiwa kwenye chama chake na amefanya hivyo kwenye bajeti za mwaka jana na mwaka huu.

"Mimi nafanya kazi kwa misimamo yangu, penye kukosoa nakosoa penye kusifia nasifia bila woga, hao wanaohama kwa hoja na migogoro ndani ya chama ni waongo kupitiliza hakuna chama chochote kisicho na migogoro lakini ni namna gani ya kukabiliana nao, hata hao CCM wana migogoro kibao lakini wanajua namna ya kuikabili nje wanahisi kuna amani", amesema Sakaya.
Ameongeza kuwa "Hakuna hoja nyingine mbovu kama kuunga jitihada za chama tawala wanaofanya hivyo ni kwa maslahi yao binafsi na sio maslahi ya taifa na mimi siwezi kufanya hivyo naheshimu sana nafasi niliyopewa na wananchi wa Kaliua, na 2020 wao ndio watakaofanya maamuzi baadaya kunipima kwa miaka mitano".

Siku za hivi karibuni, Magdalena Sakaya alitajwa kwenye orodha ya wabunge watakaohama vyama vyao na kujiunga na upinzani, suala ambalo liliibua mijadala kupitia mitandao ya kijamii, ambapo baadhi yao walisema anaweza ondoka pia kutokana na mgogoro wa chama chake cha CUF.