Jumatatu , 25th Aug , 2014

Imeelezwa kuwa nchi nyingi za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati zinapata pato kubwa katika shughuli zake za kiuchumi kupitia sekta binafsi tofauti na miaka ya nyuma ambapo fedha hizo zilitokana na makusanyo ya serikali pamoja na fedha za wahisani.

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Dkt Richard Sezibera.

Akizungumza jijini Arusha, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika mashariki Dkt. Richard Sezibera amesema sekta binafsi ndio injini ya uchumi wa Afrika Mashariki na kuongeza kuwa Jumuiya hiyo itahakikisha wananchini wa nchi wanachama wanafaidika na ukuaji wa uchumi wa jumuiya kupitia fursa za kiabiashara zinazopatika EAC.

Dkt. Sezibera amesema hayo wakati wa ufunguzi wa moja ya vitega uchumi vilivyofunguliwa jijini Arusha kupitia uwekezaji uliogharimu zaidi ya Dola za Marekani milioni 2 ambazo ni sawa na fedha za Tanzania Shilingi bilioni 3.3 na kuwawezesha vijana zaidi ya 50 kupata ajira za kudumu mkoani humo.

Aidha katika hatua nyingine, serikali imezitaka halmashauri za wilaya, miji, manispaa na majiji nchini kuongeza mapato kwa kukusanya kodi za majengo na wafanya biashara wakubwa badala ya kukimbizana na wafanyabiashara ndogondogo.

Akizingumza na wakazi wa mjini Iringa Mwishoni mwa wiki Naibu Waziri Wa Fedha Mwigulu Nchemba amesema tabia za halmashauri na serikali kushughulika na wafanyabiashara wadogo na kuwaacha wakubwa wakiendelea kukwepa kodi imepitwa na wakati.

Mwigulu ameongeza kuwa utaratibu uliopo sasa duniani kote kuongeza pato la sehemu husika ni kukusanya kodi kubwa kwa matajiri ili kutoa huduma bora kwa maskini kwa kuwaboreshea huduma mbalimbali

Aidha Mwigulu amesema mpango wa serikali hivi sasa ni kupunguza matumizi nakuongeza mapato ambapo wameanza na elimu kwa kulipa mishahara kupitia acount za walimu moja kwa moja ili kudhibiti mishahara hewa.