Jumatano , 13th Nov , 2019

Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, amesema kuwa Serikali imemsimamisha kazi Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Mbolea nchini (TFC), pamoja na kumuagiza Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya BAJUTA kuzirudisha haraka iwezekanavyo, fedha za umma kiasi cha Shilingi bilioni 4.5

alizopewa kinyume na maelekezo ya Serikali.

Naibu Waziri Bashe ametoa kauli hiyo leo Novemba 13, 2019, bungeni Dodoma, wakati akijibu swali lililoulizwa na Mbunge wa Chunya, Victor Mwambalaswa, lililokuwa likihoji nini hatma ya mbolea na viuatilifu vya zao la korosho, ambavyo licha ya Serikali kutoa pesa ni mwaka sasa umepita mbolea na viuatilifu hivyo bado viko bandarini.

Akijibu swali hilo Bashe amesema kuwa Serikali kwa sasa tayari imekwishachukua hatua stahiki na wako kwenye majadiliano na Mamlaka husika wakiwemo TPA ili kuweza kuvitoa kabla havijaharibika na kuwagawia wakulima kwa ajili ya msimu ujao.

"Ni kweli Serikali ilitoa pesa bilioni 10 kwa ajili ya kuagia viuatilifu hivyo na Serikali imemsimamisha Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya TFC kama hatua ya awali kwa uzembe huu,nitumie nafasi hii ndani ya Bunge hili, Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Bajuta kurudisha bilioni 4.5 alizopewa na tumeongea na TPA wamekubali kutuondolea gharama zote na sasa tuko katika hatua za mwisho kuvitoa viuatilifu hivyo kabla havijaharibika ili tuweze kuwagawia wakulima" amesema Naibu Waziri Bashe.

Kampuni ya Mbolea ya TFC ilipewa jukumu la kuagiza mbolea na dawa aina ya Salfa ili iweze kuuzwa kwa wakulima wa zao la Korosho kwa bei nafuu, ambapo kampuni ya Bajuta ilipewa bilioni 4.5 kati ya bilioni 10 na Bodi ya Korosho zilizotolewa na hazina kwenda kwa Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC), kinyume na maagizo ya Serikali.