Jumatatu , 15th Apr , 2024

Shirika la viwango Tanzania (TBS), limewataka wafanyabiashara na wajasiriamali wadogo nchini kutumia fungu lililotengwa na Serikali shilingi milioni 250 kwa ajili ya kuongeza viwango vya bidhaa zao ili kujiongezea wigo wa biashara zao kukubalika kimataifa.

Dkt Athuman Ngenya, Mkurugenzi Mkuu wa TBS

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt Athuman Ngenya wakati akiongea na EATV leo jijini Dar es Salaam na kuwataka kutumia fursa hiyo kuongeza thamani ya bidhaa zao.

"Serikali imetoa fungu la shilingi milioni 250 kwa ajili ya uongezaji thamani bidhaa za wafanyabiashara wadogo ambapo kwa kufanya hivyo kunawaondolea vikwazo wanapoenda nchi yoyote ya ukanda wa Afrika Mashariki kutokutana na kikwazo chochote", Dkt. Athuman Ngenya

Aidha, katika kudhibiti mianya ya bidhaa zisizo na ubora TBS imesema inashirikikana na taasisi nyingine za Serikali kuhakikisha hakuna bidhaa bandia inaingia nchini.

"Tunashirikiana na taasisi nyingine za Serikali kama TRA, FCC, TAMISEMI, Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vingine vya usalama kwahiyo kuna muda tunaambatana nao ili kuhakikisha bidhaa zinazoingia nchini ni salama" Dkt. Athuman Ngenya

Kwa upande wao wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam, wameiomba Serikali iweze kutoa elimu ya kutosha kuhusu utofauti wa bidhaa halisi na bidhaa bandia.

"Tunaiomba serikali iweze kutupa elimu ili tuweze kutofautisha kwani wengi wetu hata elimu zetu ziko chini na hatuwezi kutofautisha uhalali na ubandia wa bidhaa tunazotumia", Mariam Joseph, Mkzi wa Dar es Salaam.

"Kwenye kutofautisha hatujui sisi tukifika tunanunua tunatumia mpaka itokee madhara ndio huwa tunafuatilia" Selestine Enock, Mkazi wa Dar es Salaam.

"Uelewa wangu upo kwenye bidhaa moja tu ya maji labda utakuta umenuua chini unakuta kama imetobolewa halafu imewekewa gundi lakini kwa upande wa bidhaa nyingine sifahamu lakini natamani kuipata elimu hiyo", Almas Hassan, Mkazi wa Dar es Salaam.