Ijumaa , 22nd Mei , 2015

MKUU wa mkoa wa Mwanza, Magesa Mulongo, ameitaka mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa nchi kavu na majini (SUMATRA) kuhakikisha inafanya ukaguzi wa mara kwa mara wa vyombo katika Ziwa Victoria kwa lengo la kudhibiti ajali zisizo za lazima.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Magesa Mulongo,

Akizungumza katika kumbukumbu ya miaka 19 ya ajali ya meli ya Mv Bukoba iliyotokea Mei 21, 1996 kwenye makaburi ya pamoja yaliyopo Igoma wilayani Nyamagana jijini Mwanza, katibu tawala wa wilaya hiyo, Rahma Bakari, kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Mwanza, anasema vyombo vya majini lazima vifanyiwe uchunguzi mara kwa mara na SUMATRA.

Amesema kufanya hivyo kutasaidia kupunguza ajali zisizo za lazima na kupoteza vifo kwa wasafiri wa majini katika Ziwa Victoria.

Aidha amesema endapo mamlaka hiyo itafanya ukaguzi wa mara kwa mara tatizo la ajali litapungua na kulinda usalama wa watanzania ambao wanatumia usafiri wa majini.

Pia upakiaji wa abiria na mizigo kupitia kiasi kunaweza kusababisha ajali zisizo za lazima hivyo ni bora wafanyabiashara wasafirishaji, watumiaji wa usafiri huo kuhakikisha wanafuata kanuni na taratibu za usafiri kama zinavyoelekeza.

Mwanamitindo wa kimataifa ambaye alimpoteza mama yake katika ajali hiyo, Flaviana Matata, amesema tukio hilo ni kati ya matukio ambayo hayatasahaulika maishani mwake kutokana na kumpoteza mzazi wake huyo akiwa na umri mdogo.

Amesema tukio hilo ni tukio ambalo hawezi kulisahau katika maisha yake, na ndiyo maana anashindwa kulizungumzia zaidi ya kuwashukuru wote walioacha shughuli zao na kujumuika katika kumbukunbu hiyo.

Meli hiyo ilizama MRI 21, 1996 ikitokea Bukoba na kuua abiria zaidi ya 800.