Alhamisi , 20th Jun , 2019

Jeshi la Zimamoto na uokoaji nchini limesema kuwa ni hatari sana ikiwa mtu atatikisa mtungi wa gesi kuangalia kama bado gesi ipo ndani, kwani inaweza kutokea mlipuko mkubwa wa moto.

Mkuu wa Jeshi la Zimamoto Kamishina Jenerali Thobias Andengenye.

Tahadhali hiyo imetolewa na Mkuu wa Jeshi hilo, Kamishina Jenerali Thobias Andengenye, wakati wa zoezi la kufunga mitungi ya kuzimia moto katika Shule ya Sekondari Simiyu mjini Bariadi.

Jenerali Andengenye amesema kuwa watu wengi wamekuwa wakitikisa mitungi hiyo kuangalia kama bado gesi ipo, ambapo inaweza kusababisha kuongezeka kwa presha ya gesi na kulipuka.

Ukitikisa gesi presha yake inaweza kupanda na msukumo mkubwa na kulipuka, ni kama ilivyo kwenye soda au bia ambavyo ukatikisa unaona presha inavyopanda, ndivyo hata kwenye gesi ilivyo tunawashauri watu wasifanye hivyo ni hatari mno,” amesema Jenerali Andengenye.

Aidha amewashauri watu ambao wanataka kuangalia kama mtungi una gesi, watumie maji kwa kuweka  mtungi wa gesi kwenye maji kisha utolewe na sehemu ambayo itakauka haraka hiyo inaashiria hakuna gesi na ambayo itabaki na maji ndipo gesi ilipo.