Jumamosi , 26th Dec , 2020

TAKUKURU mkoani Mara imefanikiwa kuwarudishia wanakikudi wa Minazini, Trekta lenye thamani ya shilingi Mil. 39, ambalo lilikuwa ni mali ya kikundi hicho baada ya kikundi hicho kuchukua mkopo wa Mil. 6 hali ilipelekea mkopeshaji kulichukua trekta hilo kinyume na makubaliano ya awali.

Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Mara, Alex Kuhanda

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Mara, Alex Kuhanda, amesema kuwa trekta hilo ni mali ya serikali lililotolewa kwa kikundi hicho mwaka 2013 kwa ajili ya kuwawezesha wana kikundi kulima kisasa.

"Mkataba wa mkopo wenyewe ukiangalia masharti yake yanatia ukakasi na ulilenga kunufaisha mtu mmoja na siyo kikundi", amesema Kuhanda.

Katika hatua nyingine Kuhanda, amesema kuwa wanalishikilia gari aina ya lori lenye namba za usajili T277 AKQ, lililokuwa limebeba shehena ya mkaa na huku likiwa limekwepa kulipa ushuru wa serikali.

Aidha Kuhanda amesema kuwa kwa mwaka ujao wa 2021, watabadilisha namna ya kuwasikiliza wateja wao kwa kuanzisha huduma ya kuwafuata walipo badala ya kusubiria kuletewa malalamiko ofisini.