Jumamosi , 7th Nov , 2015

Tanzania imefanikiwa kupunguza zaidi ya asilimia 50 ya vifo vinavyotokana na uzazi kutoka vifo 102 mwaka 2010 hadi kufikia vifo 54 mwaka 2015.

Katibu mkuu wa wizara ya afya na ustawi wa jamii Dkt Donan Mmbando

Tanzania imefanikiwa kupunguza zaidi ya asilimia 50 ya vifo vinavyotokana na uzazi kutoka vifo 102 mwaka 2010 hadi kufikia vifo 54 mwaka 2015 kati ya watoto 1000 wanaozaliwa na kulifikia lengo la milenia namba 4 la miaka 5 iliyopita lililolenga kupunguza idadi ya vifo vitokanavyo na uzazi na hatimaye kuvitokomeza kabisa.

Akiongea jijini Dar es salaam kwa niaba ya katibu mkuu wa wizara ya afya na ustawi wa jamii Dkt Donan Mmbando, Mkurugenzi wa kinga Dkt Neema Rusibamayila amesema kuwa lengo hilo limefikiwa kwa serikali kushirikiana na wadau wengine wa afya ambapo mafunzo yalitolewa kwa wauguzi 200 ili waweze kutoa huduma za dharura kwa wajawazito pale inapolazimika.

Kwa upande wake mganga mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Dkt Grace Maghembe amesema kuwa katika kuendelea kuboresha huduma za afya ya uzazi serikali kwa
kushirikiana na hospitali ya CCBRT inaandaa mafunzo maalum ya dawa za usingizi zinazotumiwa wakati wa kufanya upasuaji ili kuwa na wataalam wengi zaidi na hivyo kutokomeza kabisa vifo vinavyotokana na uzazi.