Jumamosi , 19th Sep , 2015

Watu tisa wamejeruhiwa vibaya na magari mawili kuharibiwa katika vurugu ambazo zimetokea jijini Mbeya zikihusisha wafuasi wa chama cha mapinduzi, CCM, na wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo, CHADEMA.

Kamanda wa polisi mkoa wa mbeya, kamishna msaidizi mwandamizi wa polisi, Ahmed Msangi.

Tukio hilo limetokea baada ya msafara wa mgombea ubunge katika jimbo la Mbeya mjini, Joseph Mbilinyi maarufu kwa jina la Mr. II Sugu kupita jirani na mahali ulipokuwa ukifanyika mkutano wa mgombea ubunge wa CCM, Sambwe Shitambala.

Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya, kamishna msaidizi mwandamizi wa polisi, Ahmed Msangi amesema vurugu hizo zimetokea katika eneo la Mbata, kata ya Ghana jijini Mbeya wakati msafara wa mgombea ubunge wa CHADEMA, Joseph Osmond Mbilinyi ukipita katika eneo hilo ukielekea eneo la Nsowo kwa ajili ya kufanya kampeni.

Kuhusu hatua ambazo zinachukuliwa na jeshi la polisi ili kuhakikisha kuwa kampeni za uchaguzi mkuu zinaendelea na kumalizika kwa amani, kamanda Msangi anasema kuwa watuhumiwa wote bila kujali hadhi zao watafikishwa mahakani wakati wowote baada ya majalada yao kupitiwa na mwanasheria wa serikal

Aidha kamanda Msangi amevitaka vyama vyote vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi mkuu kuzingatia ratiba ya kampeni ambayo imetolewa na tume ya taifa ya uchaguzi ili kuepusha migongano isiyokuwa ya lazima ambayo pia inaweza kuhatarisha amani kwa jamii.