Jumatano , 14th Feb , 2018

Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Mhe. Freeman Mbowe amewataka wanachama wa chama hicho kuwa waangalifu juu ya usalama wao katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi ili wasiweze kudhurika na watu wenye nia mbaya nao.

Mbowe ametoa kauli hiyo wakati alivyokuwa anazungumza na waandishi wa habari juu ya kifo cha Katibu wa Kata Hananasif, Daniel John kilichotokea jana katika mazingira ya kutatanisha

"Polisi wanawaonea watu wetu, wanawauwa. Tumelalamika mara nyingi mpaka tukafikia hatua ya kususia chaguzi, tunafikili labda wenzetu wanajifunza kwa hilo. Lakini bado tunaona vyombo vya serikali, ni watu ambao wanastahili kusimamia haki kati pande zote, ndio hao hao wanakwenda kusababisha malumbano, matusi, kuwagawa wananchi, kuigawa jamii, na hadi sasa tunaonekana kuna watu kazi yao ni kuuwawa  na tunalazimika kukubali kuendelea kuuwawa", amesema Mbowe.

Pamoja na hayo, Mbowe ameendelea kwa kusema "tunawaambia wanachama wetu waendelee kuwa waangalifu, wasitembee mmoja mmoja kutokea sasa mpaka siku ya uchaguzi watembee kwa vikundi na wajiweke katika mazingira ya kujilinda wakati wote".

Kwa upande mwingine,  Mhe. Freeman Mbowe amedai vyombo vya dola vimekuwa na ubaguzi katika suala zima la kulinda usalama wa raia wake ambapo jambo hilo sio zuri kiutendaje.