Jumatano , 15th Feb , 2023

Kamati ya ulinzi na usalama mkoani Kagera imeanzisha programu maalum katika kata zote 192 ili kutoa elimu kwa kushirikiana na wadau wengine ikiwamo taasisi za kidini, lengo likiwa ni kupunguza mauaji yanayoendelea kutokea na kusababisha kuwapoteza wananchi wasio na hatia.

Mkuu wa mkoa wa Kagera Albert Chalamila

Akizungumza baada ya kutokea mauaji ya mke wa mwenyekiti wa mtaa wa National Housing, Kata ya Rwamishenye katika Manispaa ya Bukoba, Mkuu wa mkoa wa Kagera Albert Chalamila, amesema kuwa mauaji mengi yanayotokea yanafanywa na ndugu, wapenzi ama kutokana na visasi vilivyotokea miaka ya nyuma.

"Mfano katika tukio lililotokea Rwamishenye la mauaji ya mke wa mwenyekiti, inasemekana kijana aliyehusika alikirimiwa kuishi nao katika nyumba yao, lakini yale yaliyotokea katika mji wa Biharamulo ni mtu aliamka usiku akamziba pua mkewe na watoto wake wawili na kuwasababishia kifo, kwa mauaji haya polisi peke yao hawawezi, tunapaswa kushirikiana," amesema RC Chalamila

Naye Kamanda wa Polisi mkoani Kagera William Mwampaghale, amesema kuwa mauaji yapo na yanaendelea, kwa visa vilevile ikiwamo wivu wa kimapenzi na migogoro ya kifamilia ambayo yanaongoza, yakifuatiwa na yanayohusiana na migogoro ya ardhi.