Jumanne , 12th Jan , 2016

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Mohamed Ali Shein leo amewaongoza Wananchi wa Zanzibar katika sherehe za miaka 52 ya Mapinduzi ya huku akiitaka Tume ya Uchaguzi ZEC itangaze tarehe ya uchaguzi.

Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dr. Ali Mohamed Shein amesema uchaguzi wa Zanzibar wa marudio uko palepale na kinachosubiriwa ni tume ya Uchaguzi Zanzibar ZEC kutangaza siku ya kurudiwa uchaguzi.

Dr. Shein ameyasema hayo alipokuwa akihutubia mamia ya wananchi pamoja na viongozi mbalimbali waliohudhuria katika kuadhimisha miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Dkt. Shein amesema licha tume hiyo kutaja tarehe lakini juhudi za kukuza za kutafuta suluhu ya mgogoro huo bado inaendelea chini ya viongozi hivyo imewataka wananchi visiwani humo wawe watulivu na waendelee kudumisha amani.

Aidha Dkt. Shein amesema kuwa ana imani na mazungumzo hayo yatafikia muafaka kwa amani na utulivu na kupata kiongozi wanaemtaka ili wananchi wa Zanzibar waendelee na shughuli zao kama kawaida.

''Kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 na kwa sheria ya uchaguzi namba11 ya Zanzibar inatamka wazi kuwa tume ya uchaguzi ya Zanzibar kuwa ndiyo yenye jukumu la kusimamia na kuitisha uchaguzi hivyo tuisubirie'' Amesisistiza Dr Shein.

Katika hatua nyingine Dkt. Shein amesema amesema nchi hiyo imepiga hatua kubwa kiuchumi katika kipindi hicho huku juhudi za kukuza uchumi na kuboresha huduma za jamii katika visiwa hivyo zikiendelea katika kipindi kijacho.

Dkt. Shein amesema pia katika jitihada za kuimarisha uchumi visiwani huo serikali imeendelea kuboresha sekta mbalimbali za kiuchumi visiwani humo ikiwemo sekta ya viwanda, Utalii na kilimo ili kupiga hatua zaidi za kimaendeleo viswani humo.

Sherehe za mapinduzi ya Zanzibar zimehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Magufuli, Makamu wa Rais Samia Suluhu Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Marais wastaafu Ally Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na viongozi wengine waandamizi pamoja na mamia ya wananchi.

Aidha akimkaribisha Kuzungumza na wananchi makamu wa pili wa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amewashukuru wakuu wa taasisi zote za serikali na binafsi kwa kujitolea kuwapendezesha watu wa maandamano na wazanzibar kwa kujitokeza kwa wingi katika kukumbuka siku hii muhimu.