Jumanne , 1st Sep , 2015

Chama cha NCCR-Mageuzi mkoa wa Mtwara kimepinga maamuzi ya kupewa jimbo la Mtwara mjini kwa(CUF) kusimamisha mgombea ubunge kupitia (UKAWA), yaliyotolewa na Mgombea mwenza wa urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo, Juma Haji Duni.

Mgombea mwenza wa Urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo, Juma Haji Duni.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, mwenyekiti wa NCCR mkoani humo na mgombea wa ubunge katika jimbo hilo, Uledi Hassan, amesema kilichotamkwa na mgombea huyo siyo makubaliano ya UKAWA kwani makubaliano rasmi yanatolewa katika vikao halali vinavyowahusisha viongozi wakuu wa umoja huo.

Aidha, amesema iwapo taratibu za kutangazwa mgombea zitafuatwa, yuko tayari kumuunga mkono mgombea yeyote atakayepitishwa na umoja huo hata kama siyo yeye, lakini sio kwa njia ya kutangaza katika majukwaa ya mikutano ya kisiasa.

Shinikizo kutoka kwa wananchi limepelekea mgombea mwenza wa nafasi ya Urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Juma Duni Haji, kulazimika kumtangaza Maftaha Nachuma wa Chama cha Wananchi (CUF), kuwa mgombea ubunge katika jimbo la Mtwara mjini kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).

Maamuzi hayo yalitokana na wananchi waliojitokeza katika mkutano wa hadhara wa kampeni uliofanywa na UKAWA leo katika viwanja vya mashujaa mkoani humo, kuwa na shauku ya kutaka kumjua mgombea wao.