Jumatano , 28th Oct , 2015

Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) wametoa tamko lao la kupinga matokeo yanayotolewa na tume na kudai mchakato huo umejaa hujuma dhidi yao ikiwa ni pamoja na kukamatwa kwa wataalamu wa IT.

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ambae pia ni Mwenyekiti Mwenza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA)Freeman Mbowe.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam mwenyekiti mwenza wa umoja huo ambaye chama chake ndicho kilichomsimamisha mgombea urais Mh. Freeman Mbowe amesema mgombea wao anafanyiwa hujuma ikiwa ni pamoja na kuingiliwa kwa mchakato wa utoaji matokeo.

Aidha Mh. Mbowe amesema kuwa kitendo cha jeshi la polisi kuwakamata wataalamu wao ambao walikuwa wakisadia kukusanya matokeo hakikubaliki huku akisisitiza hii leo umoja huo utaitisha mkutano kutoa tamko rasmi juu ya suala hilo.

Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa CHADEMA, Prof. Safari amesema kuwa ushahidi walionao katika fomu zao unaonesha kuwa kuna baadhi ya maeneo tume imetoa matokeo ambayo hayaendani na yale waliyoyakusanya wao.

Naye mwenyekiti mwenza wa umoja huo ambaye pia ni mwenyekiti wa chama cha NCCR-Mageuzi Bw, James Mbatia amesema hujuma hizo wanazifanya hata kwenye utoaji matokeo ambapo mpaka sasa jimbo la Kigoma Kusini hawajatoa matokeo ikionesha dhahiri kuna udhalimu unaotaka kufanyika.